Sunday, March 16, 2014

Kigoma-Katavi: Usafiri wa mateso

Basi pekee linalofanya safari kati ya Kigoma na Mkoa wa Katavi kutoka katika kampuni ya Adventure Connection likiwa limenasa katika tope kufuatia mvua zinazoendelea kunyesha. Hapa ni katika eneo la Mishamo mkoani Katavi

Wednesday, August 28, 2013

Radio Imaan FM na Kwa Neema FM zarudi hewani

                                  JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA 

                                  MAMLAKA YA MAWASILIANO TANZANIA 

      
                                      TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
  
KUREJESHWA KWA URUSHAJI MATANGAZO RADIO IMAAN FM NA KWA NEEMA FM  RADIO

1.0 Utangulizi:

Mnamo tarehe 26/02/2013 Kamati ya Maudhui ya Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania ilitoa uamuzi wa kuvifungia vituo vya utangazaji vya Radio Imaan ya mjini Morogoro na Kwa Neema FM Radio ya jijini Mwanza baada ya kukiuka Sheria na Kanuni za Utangazaji.

Kamati ya Maudhui iliuita uongozi wa vituo hivyo tarehe 11/02/2013 na tarehe 14/02/2013 ili kujitetea na vyote vilikiri kosa. Baada ya kutafakari utetezi wa Radio Imaan na Radio ya Kwa Neema FM na kwa kuzingatia Sheria na Kanuni za Utangazaji, Kamati iliamua kutoa adhabu kwa vituo vyote viliwi kama ifuatavyo:-

a) Vituo vyote vilipewa onyo pamoja na kufungiwa kurusha matangazo kwa kipindi cha miezi sita kuanzia tarehe 26/02/2013;

b) Vituo vyote vilitakiwa kuithibitishia Mamlaka ya Mawasiliano na Kamati ya Maudhui kwa maandishi kuwa hawatarejea kutenda kosa la aina hiyo au linalofanana na hilo. Ikiwa vitarudia Kamati ya Maudhui haitasita kuvifutia leseni zao za utangazaji.

2.0 Kutekeleza adhabu na hatua zilizochukuliwa na vituo hivyo na Mamlaka ya Mawasiliano:

Baada ya Uamuzi huo kusomwa, vituo vyote viwili vilianza kutekeleza adhabu mara moja kama ilivyotakiwa kwa mujibu wa Sheria na Kanuni za Utangazaji. Mamlaka ya Mawasiliano ilipokea barua ya udhibitisho wa kutofanya kosa tena yaani “Commitment letter” pamoja na sera ya uhariri (Editorial Policy) na ratiba ya vipindi kutoka kwa vituo vyote viwili.

Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania ilifanya ukaguzi kwa vituo vyote viwili ili kujiridhisha na kuzipitia sera za uhariri pamoja na mwongozo wa vipindi kabla ya kuvifungulia.

3.0 Kurejeshwa kwa Matangazo

Kamati ya Maudhui iliandika barua tarehe 27/08/2013 kuhusu kuvifungulia vituo hivyo vya utangazaji vya Radio Imaan ya mjini Morogoro na Kwa Neema FM Radio ya jijini Mwanza baada ya kutumikia adhabu kwa mujibu wa Sheria na Kanuni za Utangazaji. Vituo hivi vimeanza kurusha matangazo yake kuanzia leo tarehe 28/08/2013 baada ya muda wa adhabu kuisha.

Kamati ya Maudhui inapenda kutumia fursa hii kuvionya vyombo vya habari vya utangazaji vya redio na televisheni kuwa makini katika kutekeleza masharti ya leseni pamoja na kufuata Sheria na Kanuni za Utangazaji. Kamati ya Maudhui haitasita kutoa adhabu kali au kuvifungia vituo vitakavyokiuka Masharti ya leseni, Sheria pamoja na Kanuni za Utangazaji au hata kuvifutia leseni zao.

Kamati ya Maudhui inatoa wito kwa vyombo vya habari vya utangazaji kuzingatia Sheria, Kanuni na Masharti ya leseni ilikuboresha Sekta ya Utangazaji na kudumisha amani nchini.

Eng. Margaret Munyagi
Mwenyekiti,
Kamati ya Maudhui Ya TCRA,
S.L.P. 474,
DAR ES SALAAM.
28/08/2013

 ----

KUHUSU KAMATI YA MAUDHUI: 

1.1. Kamati ya Maudhui ni kamati iliyoundwa kwa mujibu wa sehemu ya IV kifungu cha 26 (1) cha Sheria Namba 12 ya Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania ya mwaka 2003, na marekebisho yake katika kifungu 173 cha Sheria ya Mawasiliano ya Kielektroniki na Posta (EPOCA) Mwaka 2010 

Kwa mujibu wa sheria, majukumu na kazi za Kamati ya Maudhui ni pamoja na:-

(a) Kumshauri Waziri wa Sekta kuhusiana na Sera ya Utangazaji nchini; 
(b) Kushughulikia malalamiko kutoka kwa watangazaji na watumiaji wa huduma za utangazaji nchini; 
(c) Kusimamia na kuhakikisha kuwa kanuni za utangazaji zinafuatwa.
 (d) Kusimamia na kufuatilia maudhui ya vituo vya utangazaji. 

1.2. Kamati hii ilianza kazi zake Oktoba 2012 baada ya kuzinduliwa rasmi na Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo Dk. Fenella Mukangara (MB) tarehe 4 Desemba, 2012. 

1.3. Kamati ya Maudhui inaundwa na wajumbe watano. Wanne ni wateuliwa wa Waziri mwenye dhamana ya Sekta ya Utangazaji na Mwenyekiti ambaye huchaguliwa miongoni mwa wajumbe wa Bodi ya TCRA. Muundo huo umetolewa na sehemu ya 26 (2) ya Sheria ya TCRA ya Mwaka 2003.

Majina ya wajumbe ni kama ifuatavyo:-

i. Mhandisi Margareth Munyagi -Mwenyekiti
ii. Bwana Walter Bgoya -Makamu Mwenyekiti
iii. Bwana Abdul Ngarawa -Mjumbe 
iv. Bwana Joseph Mapunda -Mjumbe 
v. Bwana Yusuf Nzowa -Mjumbe