Wednesday, September 26, 2012

Mkazi Wa Iringa,Ashukuru Kupata Virusi Vya Ukimwi

 Balozi wa Marekeni Alfonso Lenhardt akiwa katika picha ya pamoja na watu wanaoishi na virusi vya UKIMWI wanaopata huduma zao katika kituo cha Alamano, cha mjini Iringa. (Picha: Frank Leonard/Habari Leo) 

MKAZI wa hapa, Eliza Muhumba anayeishi na Virusi Vya UKIMWI, ameshukuru kupata maambukizi hayo kwani yamemwezesha kupata maisha mazuri. “Maisha ni mazuri kweli kweli na watu wengine wanadhani napata fedha kwa njia ya kishirikina, ukweli ni kwamba bila kirusi nadhani nisingekuwa na maisha haya,” alisema katika uzinduzi wa Kituo cha Afya cha Alamano. Kituo hicho kilizinduliwa juzi na Balozi wa Marekani nchini, Alfonso Lenhardt na kinatoa huduma kwa watu wanaoishi na Virusi Vya UKIMWI. 

Uzinduzi wa kituo hicho kilichoanza kutoa huduma hizo mwaka 2005 kwa msaada wa Watu wa Marekani kupitia Shirika la Misaada la Marekani (USAID), ulifanyika jana. Muhumba alisema baada ya kupata ushauri nasaha na kupima afya yake katika kituo hicho cha Alamano, alianza kupata huduma za ushauri wa kisaikolojia, kisheria na msaada wa chakula, “Hiyo ilikuwa tangu mwaka 2007, nikiwa mteja katika kituo hicho zilianzishwa jumuiya za kuweka na kukopa na kwa kupitia jumuiya hizo nilianza kupata mikopo ambayo mbali na kusaidia kuboresha afya yangu, imeniwezesha kuwekeza katika shughuli mbalimbali za ujasiriamali,” alisema. 

 Alisema kwa kupitia mikopo kutoka jumuiya hiyo amejenga nyumba ya kuishi, amefungua duka la pombe na vinywaji laini, genge la chips na nyama choma na sehemu ya kunyolea nywele. Mratibu wa Kituo hicho, Christopher Kunzugala alisema Jumuiya za Kuweka na Kukopa (SILC) katika kituo hicho zina hisa zenye thamani inayokadiriwa kufikia Sh milioni 200, huku hisa moja ikiuzwa kati ya Sh 500 na Sh 10,000 kwa wanachama wa vikundi 52 vilivyoanzisha jumuiya hizo. 

Balozi Lenhardt alisema Watu wa Marekani kwa kupitia Mfuko wa Rais wa Marekani wa Kupambana na UKIMWI (PEPFAR) walianza kukisaidia kituo hicho tangu kilipoanza kutoa huduma ya uangalizi na matibabu mwaka 2005, “Kituo hicho si tu kwamba kinawapa watu fursa ya kupata huduma ya upimaji na matibabu, lakini pia kinatoa huduma za uangalizi na misaada kwa watu wanaoishi na Virusi Vya UKIMWI,” alisema. 

Alisema ushirikiano wao na kituo hicho umewezesha mpaka sasa Marekani isaidie utoaji huduma ya uangalizi na misaada kwa watu watu 2,043 wanaoishi na virusi na watu 1,795 wanaopata huduma za matibabu kituoni hapo. Aidha alisema kupitia misaada ya Watu wa Marekani, programu za “Tunajali na Pamoja Tuwalee”, wametoa mafunzo kwa waelimisharika majumbani 85. Mkurugenzi wa Kituo cha Alamano, Maria Mikela alisema kituo kimejengwa kupitia Programu ya Awamu ya Pili ya Mradi wa Tunajali unaofadhiliwa na USAID. 

                       Source: http://www.wavuti.com

No comments: